
Miaka 13 iliyopita katika siku kama leo, Hugo Chavez rais wa zamani wa Venezuela alirejea nchini kwake na kushika hatamu za uongozi baada ya kufeli jaribio la mapinduzi ya kumuondoa madarakani. Chavez Aliingia madarakani mwaka 1999 na kufanya mabadiliko makubwa kwa maslahi ya tabaka la chini. Vilevile alichukua hatua za kusimamia mashirika ya mafuta ya Kimarekani yaliyokuwa yakichimba mafuta ya nchi hiyo. Siasa za kujitegemea za Chavez ziliikasirisha sana Washington. Ni kwa sababu hiyo, ndiyo maana Marekani ilipanga na kuratibu mapinduzi mnamo tarehe 12 Machi mwaka 2002. Licha ya mapinduzi hayo kupata mafanikio katika hatua za awali, lakini wananchi wa Venezuela waliokuwa wameridhishwa na mabadiliko ya Chavez, walipinga uingiliaji wa nchi za nje katika masuala ya ndani ya nchi yao. Hugo Chavez alifariki dunia Machi 5 mwaka 2013 kutokana na maradhi ya saratani akiwa na umri wa miaka 58.
Siku kama ya leo miaka 27
iliyopita, serikali ya Umoja wa Kisovieti ilitia saini makubaliano mjini
Geneva na kukubali kuondoa majeshi yake katika ardhi ya Afghanistan.
Jeshi la Umoja wa Sovieti liliiteka na kuikalia kwa mabavu Afghanistan
mwaka 1979. Hata hivyo tangu awali majeshi hayo yalikabiliwa na upinzani
mkali wa mujahidina wa Kiafghani. Vilevile Marekani nayo iliyokuwa
ikiona maslahi yake yamo hatarini nchini Afghanistan, ilitumia wenzo wa
kijeshi, kisiasa na kiuchumi dhidi ya Moscow ili kuilazimisha iondoke
nchini Afghanistan.
Tarehe 25 Farvardin miaka 27
iliyopita serikali ya wakati huo ya Iraq ilikiri kwamba ilitumia silaha
za kemikali katika vita vyake dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Katika kipindi chote cha miaka minane ya vita hivyo Iran iliwasilisha
mashtaka katika jumuiya za kimataifa kwamba Iraq inatumia silaha za
kemikali dhidi ya wapiganaji wa Jamhuri ya Kiislamu. Wakati huo Iraq
haikukiri wala kukadhibisha habari hiyo. Hata hivyo katika siku kama hii
ya leo wakati vita vilipokuwa vimepamba moto, serikali ya Baghdad
ilikiri kwamba inatumia silaha za kemikali zikiwemo za gesi ya sumu na
hatari ya haradali dhidi ya malengo ya kijeshi na kiraia ya Iran.
Takwimu zimeonesha kwamba
utawala wa Baath wa Iraq ulifanya mashambulizi 3,500 kwa kutumia silaha
za kemikali dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kipindi chote
cha vita hivyo.
Na siku kama hii ya leo miaka
125 iliyopita muungano wa Pan American ambao baadaye ulibadili jina na
kujulikana kama Jumuiya ya Nchi za Amerika uliasisiwa. Nchi wanachama wa
jumuiya hiyo zilikuwa zikishirikiana katika nyanja mbalimbali hadi
wakati wa Vita vya Pili vya Dunia. Hata hivyo baada ya vita hivyo
kumalizika Jumuiya ya Nchi za Amerika iliundwa kutokana na kuweko haja
ya kupanuliwa zaidi mashirikiano kati ya nchi hizo. Pamoja na hayo yote
kitu kinachoitia wasiwasi jumuiya hiyo ni satwa na ushawishi mkubwa wa
Marekani katika jumuiya hiyo na hatua yake ya kukitumia vibaya chombo
hicho kwa maslahi yake ya kisiasa. Kwa sababu hiyo nchi wanachama
zinafanya jitihada kubwa za kupunguza ushawishi wa Marekani katika
jumuiya hiyo.