soundcloud

SAHAMA HAMAD 18 - Pata taarifa mbalimbali za Kisiasa, Uchumi, Dini pamoja na simulizi mbali mbali za kusikitisha zikiambatana na Makala pamoja na Tahrir za Kusisimua.. Pia tuwasiliane kupitia +255659887692 AHSANTENI...

Tuesday, 12 May 2015

ZEC YAJIBU MMAPIGO KWA MAALIM SEIF

 

 Mkurugenzi wa ZEC, Salum Kassim Ali alisema jana kuwa hakuna majina ya marehemu yanayoendelea kutumika katika Daftari la Kudumu la Wapigakura hivyo CUF iache kuipotosha jamii.
Zanzibar.

Siku moja baada ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad kutoa tuhuma nzito dhidi ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kuandikisha wapigakura wasio na sifa, tume hiyo imeibuka na kukanusha vikali.
Mkurugenzi wa ZEC, Salum Kassim Ali alisema jana kuwa hakuna majina ya marehemu yanayoendelea kutumika katika Daftari la Kudumu la Wapigakura hivyo CUF iache kuipotosha jamii.
Alikuwa anajibu madai ya Maalim Seif kuwa ZEC iliandikisha na kuruhusu wapigakura wenye umri chini ya miaka 18, walioandikishwa mara mbili, wasiokuwa wakazi na waliotumia ama majina au picha za watu wengine.
Seif ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF, alisema madai hayo yamebainika katika utafiti uliofanywa na chama hicho ili kubaini hujuma zilizofanywa na SMZ na taasisi zake ambazo zinaweza kufanyika pia katika uchaguzi ujao.
Katika majibu yake, Ali alisema sheria na taratibu za uchaguzi kabla ya kupiga kura, yaani daftari huhakikiwa na majina kubandikwa hadharani katika vituo vya kupigia kura zilifanyika, hivyo kama kungekuwa na dosari, zilipaswa kuwekewa pingamizi.
Alisema sekretarieti ya ZEC inafanya kazi zake kwa maelekezo ya makamishna wake wakiwamo wawili kutoka CUF ambao wanafanya nao kazi kwa ushirikiano mkubwa na hayakuwahi kujitokeza malalamiko hayo.
Alisema kabla ya kuanza uandikishaji mwezi huu, ZEC ilikutana na wadau vyama vya siasa na kuwaeleza mambo manne yatakayofanyika ambayo ni uandikishwaji wa mwisho kwa wapiga kura, kuhakiki daftari la wapigakura, ikiwamo kuondoa waliokufa, kubadilisha taarifa na kuhamisha taarifa za wapigakura.
Alisema endapo kungekuwa na kasoro, makamishna hao wa CUF ndiyo wangekuwa wa mwanzo kulalamika kwa vile wapo jikoni na siyo viongozi wa chama wanaolalamika kwenye vyombo vya habari.
“Kama kweli ana ushahidi wa kile anachokizungumza, kwa nini haleti malalamiko yake ZEC badala yake analalamika kwenye vyombo vya habari?” alihoji.
Mkurugenzi wa Idara ya Usajili wa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, Mohamed Juma Ame alisema viongozi wenye dhamana wanapaswa kufanya utafiti na kupata ukweli kabla ya kutoa shutuma nzito ili wananchi wapate taarifa sahihi.
Alisema kwa mujibu wa Sheria ya Mzanzibari Mkaazi, mtu yeyote kabla ya kusajiliwa, anatakiwa awe na cheti cha kuzaliwa, barua ya sheha na haiwezekani mtoto mwenye umri chini ya miaka 18 kupewa kitambulisho hicho.
Alisema kabla ya kuandikishwa kuwa mpiga kura, lazima mtu awe na kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi na masharti ya kukipata lazima awe na cheti cha kuzaliwa na sheha amtambue.

No comments:

Post a Comment